Subcribe to our RSS feeds Join Us on Facebook Follow us on Twitter Add to Circles

Alhamisi, 12 Juni 2014

TAFSIRI NA FASIHI LINGANISHI YA KISWAHILI.



TAFSIRI NA FASIHI LINGANISHI YA KISWAHILI.


Lengo la makala hii ni kuangalia kwa ufupi fasihi linganishi ya Kiswahili na tafsiri kwa kuzingatia uchambuzi wa utanzu uliofasiriwa zaidi kulingana na data zilizokusanywa huku msisitizo ukiwa katika mchango wa tafsiri katika fasihi linganishi ya Kiswahili pamoja na changamoto zitokanazo na mchakato wa tafsiri katika kufasiri matini za kifasihi.

Ili makala hii iweze kueleweka zaidi kipengele cha fasili ya dhana za msingi kama vile fasihi linganishi pamoja na tafsiri kimezingatiwa kama ifuatavyo:

Maana ya fasihi linganishi; Miongoni mwa wataalam waliofasili dhana ya fasihi linganishi ni Boldor (2003) akimrejelea Compbell (1926) anaeleza kuwa, fasihi linganishi ni taaluma inayochunguza uhusianao uliopo baina ya fasihi mbili au zaidi nje ya mipaka ya kitaifa kwa njia ya kulinganisha mfanano na msigano (tafsiri yangu).

Dhana nyingine ya msingi ni tafsiri; Kwa mujibu wa Mwansoko na wenzake (2006) tafsiri ni uhawilishaji wa mawazo katika maandishi kutoka lugha moja kwenda lugha nyingine. Hivyo, tafsiri ni miongoni mwa nyenzo muhimu katika kukuza na kusambaza fasihi kama ifuatavyo:

Tafsiri imesaidia kuingiza utanzu mpya katika fasihi andishi ya Kiswahili, kwani historia ya fasihi barani Afrika inaonesha kwamba, hapo awali jamii za kiafrika hazikuwa na utanzu huu wa fasihi. Hivyo basi, kupitia tafsiri fasihi ya Kiswahili imeweza kujitanua zaidi.

Pia tafsiri imesaidia kukuza na kusambaza fasihi ya Kiswahili ulimwenguni. Kwa mfano kiswahili kwenda lugha nyingine kama vile, Kijerumani “Kasri ya Mwinyi Fuad” (Dei Sklaverei der Gewiirze). iliyotafsiriwa na Manique Lutgens na Karin Boden (1997). Pia riwaya ya “Uhuru wa Watumwa” (The Freeing of the Slaves). iliyotafsiriwa na E.A.L.B. (1967) “Nagona na Mzingile” imetafsiriwa kwa Kifaransa na Xavier Garnier, “Bwana Myombekere na Bibi Bugonoka” imetafsiriwa kwa Kijerumani na Wilhelm J. G. Mohling nk.

Naye Ruhumbika katika makala yake (2003) anaeleza, kupitia tafsiri wasanii hukomaa kwa kusoma maandishi ya wasanii wengine na kujifunza mbinu mbalimbali ambazo zitasaidia katika kukuza na kueneza fasihi ya Kiswahili.

Vilevile mataifa mbalimbali huweza kujifunza utamaduni na historia za mataifa mengine kupitia kazi za kifasihi zilizotafsiriwa, hivyo fasihi ya taifa husika hukua na kuenea zaidi.

Lifuatalo ni jedwali la mapitio ya vitabu mbalimbali vilivyotafsiriwa kwa lugha ya kiswahili.





JINA LA KZI
UTANZU
JINA LA MFASIRI
MWAKA
LUGHA



“The Well of Gining” Kisima cha Giningi
Tamthilia
Muhamed S. Abdalla
1968
Kiingereza-Kiswahili



Maisha Yangu “Moya Zhizn”
Riwaya
Andrei Zhukov
1968
Kiswahili-Kirusi

3
Historia ya Dunia ya Kale


V. Makarenko
1988
Kirusi-Kiingereza

4
Dada Alyonushka na kaka Ivanushka
Hadithi
M. Mbigili.
2002
Kirusi-Kiswahili

5
Postamasta
Riwaya
Bernard Mapalala
2003
Kirusi-Kiswahili

6
Tufani
Tamthilia
Samuel S. Mushi
1969
Kiingereza-Kiswahili

7
“I will marry when I want” Nitaolewa Nikipenda
Tamthilia
E. A. E. P. Ltd
1982
Kiingereza-Kiswahili

8
(The list) Orodha
Tamthilia
Saifu D. Kiango
2006
Kiingereza-Kiswahili

9
(The Beautiful One are Not yet Born) Wema Hawajazaliwa
Riwaya
Abdilatifa Abdallah
1976


Kiingereza-Kiswahili

10
“The Test of Heaven” Aliyeonja Pepo
Tamthilia
M. Mkombo
1980
Kiingereza-Kiswahili

11
“The Government Inspector” Mkaguzi Mkuu wa Serikali
Tamthilia
Christon Mwakasaka


1979


Kiingereza-Kiswahili

12
Uhuru wa Watumwa “The Freeing of The Slaves in East Africa”
Tamthilia
E. A. L. B.
1967
Kiswahili-Kiingereza

13
“Anthology of Swahili Poetry” Kusanyiko la Mashairi
Ushairi
Ally Ahamed Jahadhmy
1975


Kiingereza-Kiswahili

14
“The Black Hermit” Mtawa Mweusi
Tamthilia
E. A. E. P. Ltd
1970
Kiingereza-Kiswahili

15
“Song of Lawino” Wimbo wa Lawino
Ushairi
Paul Sozigwa
1975
Kiingereza-Kiswahili




Baada ya kuangalia mapitio mbalimbali ya kazi za fasihi ya Kiswahili zilizotafsiriwa ifuatayo ni tathmini fupi ya kazi hizo;

Katika kufanya tathmini imebainika kuwa tamthilia ni utanzu unaonekana kufasiriwa sana kutokana na sababu zifuatazo:

Mwansoko (2006:46) tamthilia ni utanzu uliotafsiriwa sana kutoka na malengo makuu mawili; lengo la kuigizwa na lengo la kusomwa. Pia umefasiriwa sana kutokana na kwamba, ulikuwa ni utanzu mpya katika Afrika, hivyo wageni na wenyeji walitafsiri kwa lengo la kuutambulisha katika mazingira ya kiafrika. Vilevile umeonekana kutafsiriwa sana kutokana na urahisi wa lugha yake, kwani tamthilia hutumia maneno machache na yanayoeleweka tena bila hata ya ufafanuzi wa kina kama ilivyo katika riwaya.

Pia umefasiriwa sana kutokana na umuhimu wa maudhui yake ambayo hujibainisha katika masuala mtambuko duniani kote. Kwa mfano; tamthilia ya “Nitaolewa Nikipenda, Mtawa Mweusi” nk. maudhui yake yanahalisika katika jamii mbalimbali. Vilevile umetafsiriwa sana kwa lengo la kukuza na kueneza lugha adhimu ya Kiswahili, ambayo haikuwa na machapisho mengi yahusuyo fasihi andishi.

Kwa upande wa lugha zilizojitokeza zaidi katika kufanikisha suala la tafsiri ya fasihi ya Kiswahili ni lugha ya kiingereza, na Kiswahili; lugha ya Kiingeza imejitokeza sana katika tafsiri kutokana na kwamba, waingereza ni moja kati ya mataifa yaliyotawala sehemu kubwa ya dunia, na ndio taifa lililokuwa na dola yenye nguvu zaidi. Vilevile waingereza walishapiga hatua kubwa katika maendeleo ya fasihi ukilinganisha na mataifa mengine. Pia hata lugha ya kiingereza ni moja kati ya lugha kubwa duniani na inayofahamika na mataifa mengi.

Lugha ya Kiswahili nayo imeonekana kutafsiriwa sana kutokana na hitaji la kuwa na machapisho mengi ya kifasihi ili kukuza na kueneza fasihi ya Kiswahili. Pia ni lugha inayokua kwa kasi na inayoeleweka sana Afrika Mashariki ukilinganisha na lugha nyingine.

Pamoja na hayo yote, bado inaonekana kuwa, ushairi ni utanzu unaokabiliwa na changamoto nyingi zaidi katika kufasiri kutokana na kwamba, kwa kiasi kikubwa ushairi hutumia lugha ya mkato na ya kisanaa zaidi yenye msamiati mgumu uliosheheni taswira, ishara, lahaja, tamathali za semi pamoja na misemo, mafumbo nk. Hivyo basi, kuna uwezekano mkubwa wa kupotosha maana ya kifasihi pamoja na sanaa iliyomo katika utanzu huu.

Licha ya hayo, vilevile ugumu unasababishwa na kanuni za kiarudhi hasa katika mashairi ya kimapokeo kwani, ni vigumu sana kutafsiri ushairi huku ukizingatia urari wa vina na mizani bila kupotosha maana iliyokusudiwa.

Hivyo basi, ili kuepuka changamoto hizo ingefaa sana mfasiri anayefasiri utanzu huu awe mahiri wa lugha zote mbili, pia awe mtu mwenye upeo mkubwa katika uwanja huu na mwenye juzi mkubwa wa kutunga mashairi au naye awe kiasi fulani msanii. Hivyo haitamwia vigumu sana katika kuteua maneno mwafaka.

Baada ya kuangalia tathmini ya mapitio hayo ufuatayo ni uchambuzi wa tamthilia ya “Mkaguzi Mkuu wa Serikali” kwa muongozwa wa nadharia ya usawe wa aina matini.

Newmark (1982) matini yoyote ile ifasiriwe kwa kuzingatia aina yake. Hii ina maana kwamba, kazi itakayotokea itafanana na matini chanzi. Vilevile mbinu ya “Ulinganishaji Matini” itatumika katika kufanya uchambuzi wa kazi teule, kwani katika mbinu hii matini lengwa hulinganishwa na matini chanzi ili kubaini vipengele vya kifani na kimaudhui vilivyoongezwa, vilivyopunguzwa na vilivyopotoshwa.

Kipengele hiki kitajihusisha na uchambuzi wa tamthilia ya “Mkaguzi Mkuu wa Serikali” iliyoandikwa na Nikolai V. Gogol katika lugha ya Kirusi na kutafsiriwa katika lugha zote kuu duniani ikiwemo Kiswahili. Tafsiri ya Kiswahili imefanywa na Christon Mwakasaka kupitia tafsiri ya Kiingereza iliyofanywa na D. J. Campbell kutoka katika lugha ya Kirusi.

“Mkaguzi Mkuu wa Serikali” ni moja kati ya tafsiri za kifasihi ambazo ni bora kwa kiasi fulani katika upande wa maudhui na ni mbovu kwa kiasi kikubwa katika upande wa fani. Ubovu huu unatokana na mfasiri kutozingatia nadharia ya “Usawe wa Aina Matini”. Hali hii imesababishwa na kufasiri tafsiri, yaani kufanya tafsiri kupitia matini iliyotafsiriwa bila kutumia matini chanzi kama ifutavyo:

Mfasiri amepotosha muundo asilia wa tamthilia na kusababisha kutokea kwa tafsiri tenge/mbovu. Kwa mujibu wa Gromova (2004) tafsiri ya Kiswahili ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali iliegemea tafsiri ya Kiingereza, ambayo ilifupisha matini asilia na kuigawa tamthilia ya Gogol katika matendo matatu badala ya matano. Kitendo hiki kinapunguza ubora katika taaluma ya fasihi linganishi ya kiswahili kwa kuifanya fasihi ya kiswahili kuwa na mapungufu.

Vilevile kuna upotoshaji mkubwa katika kufasiri majina ya wahusika. Mchambuzi Gromova katika makala yake anafafanua kwamba, ni vigumu sana kutafsiri katika Kiswahili majina ya Kirusi, kwani yana maana fulani. Katika tamthilia “Mkaguzi Mkuu wa serikali” kuna wahusika wengi ambao majina yao yanasababisha msomaji Mrusi apate taswira ya tabia zao. Kwa mfano, katika tafsiri ya Kiingereza lile jina la Constables ambalo katika Kiswahili ni Askari na katika Kirusi ni “Dyerzhimorda” halina maana ileile iliyokusudiwa kwa msomaji wa Kiswahili au Kiingereza. Kwani kwa Kirusi neno “morda” ni uso wa mnyama, na neno hili linatumika kwa ajili ya mtu ambaye unataka kumdharau. Ama lile jina la jaji “Lyapkin-Tyapkin” linatokana na mwigo “lyap-tyap”, maana yake ni kufanya kazi ovyo, bila nidhamu.

Pia kuna upunguzaji wa matini: Ukilinganisha matini ya Kiingereza na matini ya Kiswahili utaona kuwa katika tafsiri ya Kiswahili mfasiri hakueleza wasifu wa wahusika wakati katika tafsiri ya Kiingereza uk.16 mfasiri ameeleza kwa kirefu wasifu wa baadhi ya wahusika. Mbinu hii kama ingeingizwa katika matini lengwa ingeleta mchango mzuri katika fasihi linganishi ya kiswahili, kwani msomaji wangepata hamasa ya kutaka kujua zaidi kuhusiana na mhusika aliyemvutia. Mbinu hii haipo kwa waandishi wengi wa fasihi ya Kiswahili.

Vilevile kuna upotoshaji mkubwa wa mandhari. Mfasiri Mwakasaka katika tamthilia ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali (uk.vi) anakiri kwa kusema kuwa “...nimekata maelezo ya jukwaani kila nilipoona kuwa si ya lazima.” Kitendo hiki hakifai kabisa katika kazi za kifasihi kwani maelezo ya jukwaani ni muhimu sana katika ujengaji wa mandhari, wahusika na dhamira. mfano katika tafsiri ya Kiingereza “ACT” 1 uk.23 kuna maelezo marefu sana yanayofafanua mandhari, wakati katika Kiswahili ONESHO LA KWANZA hakuna maelezo kama hayo.

Upotoshaji wa kipengele cha mtindo: katika matini lengwa neno “ACT” limefasiri mara mbili yaani act kama onesho uk.41 na act kama tendo uk.64, wakati katika matini chanzi “The Government Ispector” limetumika neno “ACT” mwanzo mpaka mwisho. Upotoshaji huu hauna mchango mzuri katika fasihi linganishi ya kiswahili kwani huleta mkanganyiko kwa wasomaji juu ya kipengele cha mtindo.

Upotoshaji wa jalada la kitabu. Katika matini lengwa mfasiri ameweka picha ya mtu anayedhaniwa kuwa ndiye Mkaguzi Mkuu wa Serikali, wakati katika matini chanzi hakuna picha kama hiyo. Hivyo basi, kitendo hiki kinatoa mchango hasi katika taaluma ya fasihi linganishi ya Kiswahili kwani, huifanya hadhira ifikiri kwamba hivi ni vitabu viwili tofauti.

Pamoja na mapungufu hayo mfasiri kwa kiasi kikubwa amefanikiwa sana katika kipengele cha kimaudhui, hasa katika upande wa dhamira na ujumbe. Dhamira zilizojitokeza katika matini chanzi zimejitokeza pia katika matini lengwa. kwa mfano, uongozi mbaya, rushwa, utapeli, uvivu, ukahaba, uaminifu nk. Mfano, (uk.72) Bw. Posta hakuwa mwaminifu katika kazi yake kwani alikuwa akifungua barua za watu. M/WILAYA: “Lakini uliwezaje kufungua barua ya mtu mashuhuri kama yule...” Vivyo hivyo hata katika matini chanzi suala hili linajitokeza. Mfano, (uk.88) Mayor: “But how dared you open the mail of such an important personage?” Kwa ujumla kipengele hiki cha maudhui katika fasihi linganishi ya kiswahili kina mchango mkubwa sana katika fasihi ya kiswahili kwani watunzi wa kazi za kifasihi hujifunza mbinu mbalimbali katika kuelezea masuala ya kijamii. Pia hata wasomaji kupitia kazi za fasihi zilizotafsiriwa huweza kujifunza tamaduni za mataifa mbalimbali.

Hivyo basi, pamoja na yote yaliyojadiliwa katika makala hii bado mchakato wa kufasiri kazi za kifasihi unakabiliwa na changamoto mbalimbali kama ifuatavyo:

Umahiri wa lugha zote mbili au moja kwa wafasiri; yaani lugha chanzi na lunga lengwa. Kwa mfano, Mwakasaka amefasiri kupitia tafsiri ya Kiingereza kutoka na kutomudu lugha ya Kirusi, hivyo anarudia makosa yaliyopo katika tafsiri ya Kiingereza kwenye Kiswahili.

Changamoto nyingine ni tofauti za kiutamaduni. Mambo kama dini, mavazi, mila na desturi. Kwa mfano, majina ya Kirusi huwa na maana yenye ujumbe mahususi, hivyo yanapofasiriwa katika kiswahili hupoteza ile maana halisi na kupotosha ujumbe uliokusudiwa.

Vilevile changamoto ya tofauti za kiisimu baina ya lugha mbili katika muundo wa sentensi na maumbo ya maneno. Kwa mfano muundo wa Kiingereza ni tofauti na muundo wa Kiswahili.

Pia changamoto nyingine ni kutoelewa mbinu mwafaka ya tafsiri husika, hivyo husababisha tafsiri kuwa tenge/mbovu.

Hivyo basi, ni dhahiri kwamba si rahisi kupata tafsiri iliyosahihi kwa asilimia zote, isipokuwa tunaweza kupata tafsiri bora kama tu wafasiri wa kazi za kifasihi watakuwa na sifa stahiki.

Kwa mfano, uwezo wa kumudu lugha, kujua utamaduni wa lugha husika pamoja na mazingira yake, kuwa na ujuzi wa taaluma husika kabla ya kufasiri nk. Kwa misingi hii tunaweza kupata tafsiri za kifasihi zilizobora zaidi


MAREJEO

Boldor, A. (2003). etd.lsu.edu/docs/available/etd-0408103.../Boldor_thesis.pdf “Perspectives on comparative literature”. Babes-Bolyai University, Cluj. May 2003.

Gogol, N. (1836). The Government Inspector. (Translated & adapted by D.J.Campbel 1974). East African Educational Publishers. Nairobi.

Gogol, N. (1836). The Government Inspector. (Mkaguzi Mkuu wa Serikali 1979). Kimetafsiriwa na Christon Mwakasaka. East African Educational Publishers. Nairobi.

Gromova, N.V. (2004). “Tafsiri Mpya za Fasihi ya Kirusi katika Kiswahili”. Swahili forum11 (2004): 121-125.

Newmark, P. (1982). Approaches to Translation. Oxford. Pergamon Press. London.

Ruhumbika, G. (2003). “Tafsiri za Fasihi za Kigeni Katika Ukuzaji wa Fasihi ya Kiswahili.” Makala za Semina ya Kimataifa ya Waandishi wa Kiswahili III (2003). TUKI. Dar es Salaam.

Mwansoko, H.J.M na wenzake. (2006). Kitangulizi cha Tafsiri: Nadharia na Mbinu. TUKI. Dar-es-salaam.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni