Subcribe to our RSS feeds Join Us on Facebook Follow us on Twitter Add to Circles

Alhamisi, 22 Mei 2014

AINA ZA MANENO KATIKA LUGHA YA KISWAHILI.

  1. Nomino.

Nomino ni neno linalosimamia jina la kitu, mtu, mnyama, mahali, hali na kadhalika.

Aina za Nomino
  • Nomino za Kawaida
Haya ni majina ya kawaida yanayoweza kutumiwa kurejelea vitu mbalimbali, watu, wanyama, mahali na kadhalika. Nomino hizi zinaweza kuwa katika umoja au wingi kulingana na ngeli yake.
Kwa mfano nyumba, mbuzi, daktari, soko, kalamu, jua

  • Nomino za Kipekee
Haya ni majina maalum ya watu, mahali, bidhaa, kampuni, na kadhalika. Herufi ya kwanza ya nomino hizi huwa ni herufi kubwa. Nomino za kipekee haziwezi kubadilika, na hivyo basi hazina wingi.
Kwa mfano Tanzania, Nairobi, Anita, Gafkosoft, Athi, Kimbo, 

Tanbihi: Nomino ya kawaida inapotumika kutangulia au kurejelea nomino ya kipekee moja kwa moja, huandikwa kwa kutumia herufi ya kwanza kubwa. 
Kwa mfano Mlima Kilimanjaro, Waziri Mwasimba,  Chifu Mtesi, Mwalimu Makunza, Daktari Maraka

  • Nomino za Jamii
Nomino za jamii hurejelea kundi la vitu au wanyama, kwa ujumla. Aghalabu vitu vinavyorejelewa hutokea kwa makundi ya vitu mbili au zaidi. Nomino hizi hutumia wingi tu tunaporejelea makundi zaidi ya moja.
Kwa mfano  jozi la viatu, umati wa watu, bustani la maua, bunga la wanyama

  • Nomino za Wingi
Nomino hizi hurejelea vitu ambavyo hutokea kwa wingi na haziwezi kuhesabiwa. Vitu kama hivyo hutumia aina nyingine ya vipimo ili kurejelea kiasi chake. Nomino za wingi hazina umoja.
Kwa mfano maji, maziwa, changarawe, pesa, nywele

Tanbihi: Hauwezi kuhesabu pesa lakini unaweza kuhesabu sarafu za pesa kama vile shilingi, dola n.k 

  • Nomino za Vitenzi Jina
Nomino hizi huundwa kutokana na vitenzi kwa kuongeza kiungo KU mwanzoni mwa mzizi wa kitenzi.
Kwa mfano  kulima, kuongoza, kucheza, kulala
  • Kutembea kwake kutamfanya aanguke
  • Kuimba huku kunapendeza mno
  • Nomino za Dhahania

Haya ni majina ya hali au vitu ambavyo havionekani wale haviwezi kushikika. 
Kwa mfano  upendo, furaha, imani, elimu, ndoto, mawazo, maisha, usingizi

 2.Vitenzi

Vitenzi ni maneno yanayosimamia kitendo. Kila kitenzi huwa na shina la kitenzi (sehemu ndogo zaidi ya kitenzi ambayo ndiyo huwakilisha tendo hilo). Shina la kitenzi huambatanishwa na viambishi ili kutoa maana iliyokusudiwa kama vile mtendaji, mtendewa, wakati kitendo kinafanyika na pia kauli ya kitenzi hicho.
Angalia pia Mnyambuliko wa Vitenzi
Aina za Vitenzi
  1. Vitenzi Halisi
  2. Vitenzi Visaidizi + Vitenzi Vikuu
  3. Vitenzi Vishirikishi
  4. Vitenzi Sambamba

Vitenzi Halisi
Hivi ni vitenzi vinavyorejelea kitendo moja kwa moja. Vitenzi hivi haziambatanishwi na vitenzi vingine katika sentensi. Vitenzi halisi vinaweza kuambatanishwa na vitenzi 
Kwa mfano soma, kula, sikiza
  • Waziri Mwasimba aliwasili jana kutoka ng'ambo.
  • Kawia atapikia wageni.
  • Funga mlango wa dirisha.
Vitenzi Visaidizi na Vitenzi Vikuu
Vitenzi visaidizi hutumika kusaidia vitenzi vikuu katika sentensi ili kuleta maana inayokusudiwa kulingana na wakati au hali. 
Kwa mfano -kuwa, -ngali, 
  • Jua lilikuwa limewaka sana.
  • Bi Safina angali analala


Vitenzi Vishirikishi
Vitenzi vishirikishi hutumika kuelezea hali iliyopo au mazingira. Kuna aina mbili za vitenzi vishirikishi:

a) Vitenzi Vishirikishi Vikamilifu - havichukua viambishi vyovyote.
Kwa mfano ni, si, yu
  • Kaka yako ni mjanja sana. 
  • Huyo si mtoto wangu!
  • Paka wake yu hapa.
b) Vitenzi Vishirikishi Vipungufu - huchukua viambishi vya nafsi au ngeli. Vitenzi hivi vinaweza kusimama peke yake au vinaweza kufuatiliwa na vitenzi vikuu.
Kwa mfano ndiye, ndio, ndipo
  • Sanita ndiye mkurugenzi wa kampuni
  • Huku ndiko kulikoibiwa

Vitenzi Sambamba
Vitenzi vikuu viwili au zaidi vinapoandamana katika sentensi huitwa vitenzi sambamba. Aghalabu mojawapo ya vitenzi hivi hutumia viungo vingine kama vile KI, KA, PO, KU n.k
Kwa mfano -  alicheka akioga, alikula akashiba
  • Kidori alilima akachoka.
  • Mama ameenda kumtafuta baba.
  • Mwalimu alikuwa ameanza kufundisha Juma alipoingia darasani.



3.Viwakilishi

Viwakilishi vya Nomino ni maneno yanayotumika badala ya nomino. Kiwakilishi hakiwezi kuambatanishwa na nomino inayorejelewa.
Aina za Viwakilishi

Viwakilishi vya Nafsi
Viwakilishoi hivi hutumika kwa niaba ya nafsi kwa umoja na kwa wingi
Kwa mfano mimi, wewe, yeye, sisi, nyinyi, wao
Nafsi Umoja Wingi
Nafsi ya Kwanzamimisisi
Nafsi ya  Piliwewenyinyi/ninyi
Nafsi ya Tatuyeyewao
  • Sisi tuliwatangulia nyinyi kufika hapa.
  • Mimi si mjinga kama vile yeye anavyofikiria
Viwakilishi Viashiria
Viwakilishi viashiria (vionyeshi) hutumika badala ya nomino kwa kutumia kuonyesha nomino inayorejelewa bila kuitaja.    
Kwa mfano  huyu, yule, hapa, n.k
  • Hiki hakina maandishi yoyote.
  • Hao hawajui tofauti ya viwakilishi na vivumishi
  • Tumekuja hapa ili kuwaburudisha kwa nyimbo tamu tamu.


Viwakilishi Visisitizi
Hutumika kwa niaba ya nomino kwa kutumia kiashiria chake mara mbili mfululizo.
Kwa mfano yuyu huyu, wawa hawa, kiki hiki, papo hapo, mumu humu, 
  • Zizi hizi ndizo zilizovunjika wiki jana
  • Yule yule aliyekamatwa juzi, ameiba tena


Viwakilishi vya Sifa
Husimama badala ya nomino kwa kurejelea sifa yake.
Kwa mfano  -eupe, -zuri, -tamu, -embamba, -rembo
  • Vyekundu vimehamisha
  • Warembo wamewasili.
  • Kitamu kitaliwa kwanza.

Viwakilishi vya Idadi
Hutumika kusimama badala ya nomino kwa kurejelea idadi yake.
a) Idadi Kamili - hutumia nambari kuelezea idadi ya nomino
Kwa mfano saba, mmoja, ishirini
  • Wawili wamepigwa risasi polisi leo jioni.
  • Alimpatia mtoto wake hamsini kununua chakula
b) Idadi Isiyodhihirika - huelezea kiasi cha nomino kwa ujumla, bila kutaja idadi kamili
Kwa mfano chache, nyingi, kadhaa, kidogo, wastani
  • Tutazungumza na wachache kabla ya kuanzisha maonyesho yetu.
  • Kadhaa zimeripotiwa kupotea.


Viwakilishi Viulizi
Viwakilishi viulizi hutumika kwa niaba ya nomino katika kuulizia swali.
Baadhi ya viwakilishi viulizi huchukua viambishi vya ngeli
Kwa mfano -ngapi?, -pi?
  • Vingapi vinahitajika? - kuulizia idadi
  • Zipi zimepotea? 

Kunavyo viwakilishi viulizi vingine ambavyo havichukui viambishi vyovyote.
Kwa mfano wapi?, gani?,  nini?, vipi?
  • Gani imefunga bao hilo?
  • Wapi hapana majimaji?
  • Yule mvulana alikupatia nini?
  • Uliongea naye vipi? - kuulizia namna

Viwakilishi Vimilikishi
Viwakilishi hivi hurejelea nomino kwa kutumia vimilikishi.
Kwa mfano  -angu, -ako, -ake, -etu, -enu, -ao 
  • Kwetu hakuna stima.
  • Lake limekucha.
  • Zao zimeharibika tena
Viwakilishi Virejeshi
Hutumia O-rejeshi kurejelea na kusimamia nomino
Kwa mfano ambaye, ambao, ambalo, ambacho, huyo, yule
  • Ambalo lilipotea limepatikana.
  • Ambaye hana mwana, aeleke jiwe
Viwakilishi Vya A-Unganifu

Huwakilishi nomino kwa kutaja kinachomiliki nomino hiyo. Huundwa kwa kuambatanisha kiambishi cha nafsi/ngeli pamoja na kiambishi -a cha a-unganifu, kisha nomino nyingine
Kwa mfano cha, la, kwa, za, ya
  • Cha mlevi huliwa na mgema
  • Za watoto zitahifadhiwa.


Muundo wa Vitenzi
  1. Vitenzi vya Silabi Moja
  2. Vitenzi vya Kigeni
  3. Vitenzi vya Kawaida
Vitenzi vya Silabi Moja
Hivi ni vitenzi vyenye silabi moja pekee. Ili kuleta maana kamili, vitenzi hivi huambatanishwa na kiungo KU- katika kauli ya kutenda. Kama vitenzi vingine, vitenzi vya silabi moja vinaweza kunyambuliwa.

mfano:
  • -cha - kucha - jua linapochomoza asubuhi k.m kumekucha 
  • -fa kufa - kuacha kupumua, kupoteza uhai  k.m amekufa 
  • -jakuja - fika mahali hapa k.m nimekuja  
  • -lakula - kutia chakula mdomoni k.m anakula
  • -nyakunya - kutoa mabaki ya chakula toka tumboni k.m mtoto amekunya  
  • -nywakunywa - kutia kinywaji kama vile maji au maziwa mdomoni k.m ninakunywa uji
  • -pakupa - kumkabithi/kumpatia mtu kitu k.m amenipa pesa
  • -pwakupwa - kujaa hadi pomoni - k.m kisima kimekupwa maji
  • -takuta -   
  • -twakutwa - jua linapozama magharibi na usiku kuingia  k.m kumekutwa 
  • -wakuwa - kutokea katika hali au mahali fulani  k.m alikuwa 
Angalia mengi zaidi kuhusu vitenzi vya silabi moja katika ukurasa huu wa Mnyambuliko




Vitenzi Vya Kigeni
Hivi ni vitenzi vyenye asili kutoka kwa lugha nyingine badala ya Kibantu. Baadhi ya lugha hizo ni Kiarabu, Kizungu, Kireno, Kihispania n.k. Vitenzi hivi havifuatilii muundo wa kawaida wa vitenzi vya Kiswahili ambavyo huishia kwa sauti -a. Badala yake, vitenzi hivi huishia kwa sauti nyingine kama vile -e, i, -o, na u

mfano:
  • haribu
  • tubu
  • shukuru
  • salimu
  • thamini
  • amini
  • samehe
  • baleghe

Vitenzi Vya Kibantu
Hivi ni vitenzi vyenye asili ya Kibantu na ambavyo huishia kwa sauti -a. Kitengo hiki hujumuisha asilimia kubwa zaidi ya vitenzi vya Kiswahili
mfano:
  • simama
  • shika
  • tembea
  • beba
  • soma
  • lia



























4.Vivumishi


Vivumishi au visifa ni maneno yanayotuelezea zaidi kuhusu nomino. Aghalabu vivumishi hutanguliwa na nomino. 
Aina za Vivumishi

Vivumishi vya Sifa
Hivi ni vivumishi ambavyo hutoa sifa ya kitu, mtu, mahali, n.k
Kwa mfano kizuri, kali, safi, mrembo
  • Yule mama mweusi hupika chakula kitamu.
  • Mvulana mkorofi aliadhibiwa na mwalimu kutokana na tabia zake mbaya.
  • Sauti nzuri humtoa nyoka mkali pangoni
Vivumishi Vimilikishi
Vivumishi hivi hutumika kuonyesha nomino inamiliki nyingine. Mizizi ya vivumishi hivi huundwa kulingana na nafsi mbalimbali.  -angu, -ako, -ake, -etu, -enu, -ao
Kwa mfano changu, lako, yake, kwetu, vyenu, zao
  • Nitatumia talanta zangu kwa manufaa ya taifa letu.
  • Aliweka kitabu chako sebuleni mwako
  • Katosha amepata nguo yake miongoni katika sanduku lao.

Vivumishi vya Idadi
Hutueleza zaidi kuhusu kiasi, au idadi ya nomino. Kuna aina mbili za vivumishi vya idadi.
a) Idadi Kamili - hutumia nambari kuelezea idadi ya nomino
Kwa mfano tatu, mbili, kumi
  • Msichana mmoja amewauwa nyoka wawili
  • Siku kumi zimepita tangu Bi Safina alipojifungua watoto watatu
b) Idadi Isiyodhihirika - huelezea kiasi cha nomino kwa ujumla, bila kutaja idadi kamili
Kwa mfano chache, nyingi, kadhaa, kidogo, wastani
  • Watu wachache waliohudhuria mazishi ya Kajuta walikula chakula kingi sana.
  • Baba yao alikuwa mateka kwa miaka kadhaa



Vivumishi Viulizi
Vivumishi viulizi hutumika kuuliza swali. 
Baadhi ya vivumishi viulizi huchukua viambishi vya ngeli
Kwa mfano -ngapi?, -pi?
  • Ni walimu wangapi wamefukuzwa? - kuulizia idadi
  • Je, ni dawati lipi lenye funguo zangu? 

Kunavyo vivumishi viulizi vingine ambavyo havichukui viambishi vyovyote.
Kwa mfano wapi?, gani?
  • Unazungumza kuhusu kipindi gani?
  • Je, mmefika mahali wapi? - kuulizia mahali



Vivumishi Viashiria / Vionyeshi
Vivumishi viashiria hutumika kuonyesha au kuashiria nomino kulingana na mahali.
Kwa mfano 
Karibu -  hapa, huyu, hiki, hili, huku, haya, ule, wale, pale
Mbali kidogo - hapo, huyo, hiyo, hicho
Mbali zaidi - pale, lile, kile, 
  • Msichana huyu ni mkubwa kuliko yule
  • Jani hili la mwembe limekauka
  • Tupa mpira huo
Vivumishi Visisitizi
Husisitiza nomino fulani kwa kurudia rudia kivumishi kiashiria
Kwa mfano yuyu huyu, wawa hawa, kiki hiki, papo hapo, mumu humu, 
  • Jahazi lili hili
  • Wembe ule ule
  • Ng'ombe wawa hawa
Vivumishi Virejeshi
Hivi ni vivumishi ambavyo hurejelea nomino. Vivumishi hivi vinaweza kuwa vivumishi vya O-rejeshi au vivumishi viashiria vinapotumika kurejelea nomino.
Kwa mfano ambaye, ambao, ambalo, ambacho, huyo, yule
  • Msichana ambaye alikuja ni Sheila
  • Sauti ambayo uliisikia ilikuwa ya Mzee Kasorogani
  • Mti ule mkubwa umeanguka.
Vivumishi vya KI-Mfanano
Vivumishi vya KI- ya Mfanano hutumika kulinganisha sifa ya nomino na hali au tabia nyingine.  Vivumishi hivi hutanguliwa na nomino, kiunganishi cha A-unganifu na huchukua kiungo KI.
Kwa mfano  wa kifalme, za kijeshi, ya kitajiri, n.k
  • Chifu wa Vikwazoni anaishi maisha ya kimasikini
  • Chali anapenda kusikiliza mziki wa kizungu
  • Bi Naliza huvulia mavazi ya kifalme.


Vivumishi Vya A-Unganifu
Vivumishi hivi hutuelezea zaidi kuhusu nomino kwa kuonyesha kitu kinachomiliki nomino hiyo. Huundwa kwa kuambatanisha kiambishi cha nafsi/ngeli pamoja na kiambishi -a cha a-unganifu, kisha nomino
Kwa mfano cha, la, kwa, za, ya
  • Watoto wa mwalimu mkuu wana tabia nzuri
  • Chai ya daktari imemwagika


5.Vielezi.


Vielezi ni maneno yanayotoa habari zaidi kuhusu kitendo kilivyofanyika. Pia vielezi hutoa habari zaidi kuhusu hali, vivumishi na vielezi vingine.
Aina za Vielezi


  1. Vielezi vya Namna
  2. Vielezi vya Mahali
  3. Vielezi vya Idadi
  4. Vielezi vya Wakati

Vielezi vya Mahali

Vielezi vya mahali hutoa habari kuhusu mahali ambapo kitendo kilifanyika. Aghalabu vielezi hivi huundwa kwa kutumia jina la mahali au kwa kuongeza kiungo -NI mwishoni mwa neno linaloashiria mahali.
Kwa mfano nyumbani, kazini, shuleni
  • Mtoto huyo hajatulia nyumbani tangu alipotoka Mombasa.
  • Msipitie sokoni mkienda kanisani.
Vielezi vya Wakati
Huelezea zaidi kuhusu wakati kitendo kipofanyika
Kwa mfano jioni, jana, asubuhi, saa saba, mwaka juzi
  • Mzee Kasorogani amesema kwamba ataoga mwaka ujao
  • Musa alilazimishwa kuchimba mtaro saa sita usiku
  • Kisaka na Musa watakutana kesho


Vielezi vya Idadi/Kiasi
Vielezi vya idadi hutulezea kitendo kilifanyika mara ngapi

a) Idadi Kamili - hutaja idadi kamili ya mara ngapi kitendo kilifanyika
Kwa mfano mara mbili, siku mbili kwa juma, mara kumi
  • Gibi alimzaba kofi mara tatu na kisha akakimbia.
  • Daktari alimwagiza mama huyo achukue dawa mara tatu kwa siku  na arudi hospitalini siku mbili kwa mwezi
b) Idadi Isiyodhihirika - huelezea kiasi cha nomino kwa ujumla, bila kutaja idadi kamili
Kwa mfano mara chache, mara kwa mara, mara nyingi, mara kadhaa
  • Mwizi wa kuku alipigwa mara kadhaa kabla ya kuokolewa na polisi.
  • Yeye hunipigia simu mara kwa mara



6.Viunganishi.

 

Viunganishi ni maneno yanayoutumika kuunganisha, kulinganisha au kuonyesha uhusiano wa dhana mbili au zaidi.

Viunganishi vya A-Unganifu (Vimilikishi)Viunganishi vya ngeli huundwa kwa kufungamanisha viambishi viwakilishi vya ngeli pamoja na kiungo -a
Kwa mfano:
    • wa
    • la
    • za
    • vya
    • mwa
    • pa
    • cha
    • ya
  • Kiungo KWA-  hutumika kuonyesha umiliki wa mahali, sababu, ala/kitumizi, mbinu na kadhalika. Soma ukrasa huu ili ujue matumizi zaidi ya kiungo KWA

Kujumuisha
Kwa mfano:
    • Na
    • Pia
    • Pamoja na
    • Licha ya 
    • Fauka ya
    • Zaidi ya
    • vilevile

Kuonyesha Tofauti - Jambo kufanyika kinyume na matarajio
    • bila - 
    • bali -
    • ila - 
    • lakini - 
    • tofauti na - 
    • kinyume na - 
    • hata hivyo - 
    • ingawa - 
    • ingawaje - 
    • japo
    • ijapokuwa
    • ilhali
    • ijapokuwa
    • minghairi ya
    • dhidi ya


Kuonyesha Sababu

    • ili
    • kwa
    • kwa vile
    • kwa maana
    • kwa kuwa
    • kwani
    • kwa minanjili ya
    • maadam
    • madhali



Kuonyesha Matokeo

    • basi
    • kwa hivyo
    • hivyo basi
    • ndiposa
Kuonyesha Kitu kimoja kama sehemu ya kingine

    • Katika
    • Miongoni mwa
    • Baadhi ya
    • Mojawapo ya

Kuonyesha Kitendo kufanyika baada ya kingine

    • Kisha
    • halafu
    • basi


Kuonyesha Kitu kufanyika badala ya kingine

    • Badala ya
    • kwa niaba ya
    • kwa
Kulinganisha

    • Kama
    • Kuliko
    • Sawa na
    • Vile




Kuonyesha uwezekano

    • Labda
    • Pengine
    • Ama
    • Au
    • huenda










Kuonyesha Masharti

    • Ikiwa
    • Iwapo
    • bora
    • Al muradi

7.Vihusishi.

Vihusishi ni maneno yanayotuarifu zaidi kuhusu uhusiano wa nomino na mazingira yake
Kuna aina mbili za Vihusihi
  1. Vihusishi vya Mahali
  2. Vihusishi vya Wakati

Vihusishi vya Mahali
  • Juu ya
  • Chini ya
  • Kando ya 
  • Karibu na
  • Mbali na
  • Mbele ya
  • Nyuma ya
Vihusishi vya Wakati
  • Kabla ya
  • Baada ya

8.Vihisishi.

Vihisishi (I) ni maneno yanayotumika kuonyesha hisia kama vile hasira, furaha, mshangao n.k


Mifano ya Vihisishi
  • Lo!
  • Salaale!
  • Masalale!
  • Kumbe!
  • Po!
  • Ng'o!
  • Hata!
  • Akh!
  • AkaI
  • Ah!
  • Ala!
  • Haha!
  • Haya!
  • Ehee!
  • Hmmm!
  • Ebo!
  • Kefule!
  • Wee!
  • La!
  • Hoyeee!
  • Huraa!




Vielezi vya Namna

Huelezea jinsi au namna kitendo kinavyofanyika. Kitendo kinaweza kufanyika kwa namna mbalimbali. Hivyo basi kuna aina mbalimbali za vielezi vya namna:

    
a) Vielezi Halisi
Hutufahamisha jinsi kitendo kinavyofanyika kwa kutumia maneno halisi (bila kuambatanishwa na maneno mengine au viambishi vingine). 
Kwa mfano  vizuri, ovyo, haraka,
    • Kioo cha bibi harusi kilianguka na kuharibika vibaya
    • Mama alipika chakula upesi
    • Amepigwa kalamu kwa kufanya kazi kiholela
b) Vielezi Hali
Hutufahamisha hali ambayo kitendo kilifanyika. Vielezi hivi hujihusisha na tabia ya kitu/mtendaji wa kitendo 
Kwa mfano kwa furaha, kwa makini, 
  • Bibi harusi aliingia kanisani kwa madaha
  • Mtoto alilia kwa maumivu mengi
c) Vielezi Vitumizi/ala
Hutoa habari kuhusu kifaa, ala au mbinu iliyotumiwa kufanya kitendo fulani
Kwa mfano kwa kisu, kwa jembe, kwa meno, kwa moto, kwa maji
  • Mkulima aliangusha mti mkubwa kwa shoka
  • Mzee huyo alimpiga mke wake kwa bakora kabla ya kuchoma nguo zake kwa makaa
d) Vielezi Vikariri
Husisitiza kitendo kinavyofanyika kwa kutaja kielezi kinachorejelewa mara mbili mfululizo. 
Kwa mfano  haraka haraka, ovyo ovyo, juu juu
    • Polisi walipoingia, wezi walitawanyika haraka haraka.
    • Wanafunzi wengi hufanya kazi yao ovyo ovyo
e) Vielezi Mfanano
Vielezi mfanano hutumia KI-mfanano kuelezea kitendo kinavyofanyika kwa kulinganisha.
Kwa mfano kitoto, kiungwana,  
  • Babake huongea kiungwana.
  • Harida hutembea kijeshi
f) Vielezi Viigizi
Vielezi hivi huigiza sauti au mlio wa kitu, kitendo kitendo kilipofanyika kwa kutumia tanakali za sauti
Kwa mfano tuli, chubwi, tifu, chururu, 
  • Mwanafunzi alitulia tuli mwalimu alipomzaba kofi pa!
  • Kaswimu aliangusha simu changaraweni tifu na kujitumbukiza majini chubwi
g) Vielezi vya Vielezi
Vielezi hivi hutumika kuelezea kielezi kingine. Hivyo basi, hutanguliwa na kielezi badala ya kitendo. 
Kwa mfano  sana, kabisa, hasa, mno, 
    • Mamake Kajino alitembea polepole sana.
    • Chungu kilivunjika vibaya kabisa
h) Vielezi vya Vivumishi
Hutoa habari zaidi kuhusu kivumishi
Kwa mfano sana, kabisa, hasa, mno 
  • Yeye ni mrefu sana
  • Mtoto wake ana tabia nzuri mno
 

Jumatatu, 19 Mei 2014

FANI NA MAUDHUI KATIKA FASIHI


FANI NA MAUDHUI KATIKA FASIHI
FANI: huu ni ufundi wa kisanaa autumiao msanii katika kutoa ujumbe wake kwa hadhira iliyokusudiwa. Katika fani kumegawanyika vipengele mbalimbali kama vile wahusika, mitindo, muundo, mandhari, matumizi ya lugha, kufaulu na kutokufaulu kifani. Vipengele muhimu vinavyoangaliwa ni hivi vifuatavyo:
Mtindo; hii ni mbinu ya kipekee kifani na kimaudhui, zinazotofautisha msanii mmoja na mwingine.
Muundo; huu ni mpangilio wa kiufundi anaoutumia mwandishi katika kupangilia kazi yake.
Wahusika; hawa ni watu au viumbe ambavyo mwandishi wa fasihi huwatumia ili kufanikisha ujumbe kwa jamii husika. Katika kazi ya fasihi mwandishi huwagawa wahusika katika makundi mawili yaani wahusika wakuu na wahusika wadogo.
Wahusika wakuu ni wale ambao wanajitokeza kuanzia mwanzo mpaka mwisho wa kazi ya fasihi. Wahusika wadogo ni wale wote ambao wanajitokeza sehemu mbalimbali katika kazi ya fasihi kwa mfano, mwanzoni mwa kitabu hadi mwishoni mwa kitabu.
Mandhari; hii ni sehemu ambayo matukio ya hadithi au masimulizi hutokea. Mandhari huweza kuwa halisi au ya kufikirika.
Maudhui; Maudhui katika kazi ya fasihi ni jumla ya mawazo yote yanayozungumzwa pamoja na mtazamo wa mwandishi juu ya mawazo hayo. Maudhui hujumuisha mawazo pamoja na mafunzo mbalimbali yaliyomsukuma msanii hadi akatunga na kusanii kazi fulani ya kifasihi. Vipengele vya maudhui ni pamoja na dhamira, migogoro, falsafa ujumbe na msimamo.
Dhamira; hili ni wazo kuu au mawazo mbalimbali yanayojitokeza katika kazi ya fasihi. Senkoro anataadharisha maana hii isichanganywe na maudhui kwani dhamira ni sehemu tu ya maudhui na aghalabu dhamira kuu ndio hujenga kiini cha kazi ya fasihi. Dhamira zimegawanyika katika makundi mawili, kuna dhamira kuu na dhamira ndogondogo.
Migogoro; ni mivutano na misuguano mbalimbali katika kazi za fasihi. Migogoro inaweza kuwa kati ya wahusika, familia zao, matabaka yao, au hata katika nyadhifa mbalimbali.
Vilevile migogoro yaweza kuwa ya kiuchumi, kijamii, mogogoro ya nafsi, na migogoro ya kisiasa ambayo hujitokeza katika mitazamo tofauti kulingana na mtiririko wa visa na matukio yanavyopangwa na mwandishi.
Kwa ujumla suluhisho la migogoro yote ni jamii kuwa na haki na usawa kuondoa chuki, kuondokana na uvivu, kushirikiana katika kuwafichua wale wanaotumia mali ya umma kwa kujinufaisha wenyewe.
Ujumbe; mwandishi anapoandika kazi yake huwa na ujumbe ambao hutaka uifikie jamii aliyoikusudia. Ujumbe katika kazi fasihi ni mafunzo mbalimbali ambayo hupatikana baada ya kusoma kazi ya fasihi. Katika kazi ya fasihi dhamira kuu hubeba ujumbe wa msingi na dhamira ndogondogo hubeba ujumbe ambao husaidia kuujenga au kuupa uzito zaidi ujumbe wa msingi.
Msimamo; katika kazi ya fasihi, mawazo, mafunzo na falsafa ya msanii hubainisha msimamo wake kuhusu masuala mbalimbali ya kijamii. Msimamo ni ile hali ya mwandishi kuamua kufuata na kushikilia jambo fulani. Jambo hili huweza kukataliwa na wengi lakini akalishikilia tu. Msimamo ndio huweza kuwatofautisha wasanii wawili au zaidi wanaoandika kuhusu mazingira yanayofanana.
UHUSIANO WA FANI NA MAUDHUI KATIKA FASIHI
Fani na maudhui ni dhana mbili ambazo hazitenganiki. Kuna mitazamo miwili ambayo inajaribu kutazama uhusiano wa fani na maudhui katika kazi za fasihi andishi. Mitazamo hiyo ni ya kidhanifu na kiyakinifu.
Katika mtazamo wa kidhanifu wapo wataalam mbalimbali ambao wametoa maelezo yao kuhusu uhusiano wa fani na maudhui katika kazi za fasihi andishi.
Tukianza na Bi. Materu, yeye anasema fani na maudhui ni kama mwili na nguo hivyo anatoa maoni kuwa fani na maudhui ni dhana ambazo zinaweza kutenganishwa kama vile mwili unavyoweza kutenganishwa na nguo. Bi. Materu anasema maudhui ni mwili ambao ndilo umbo la ndani la kazi ya fasihi, wakati nguo ndio fani ambayo ni umbo la nje la kazi ya fasihi.
Fauka ya hayo Mtaalam mwingine ni Penina Muhando (Mlama), anasema kuwa fani na maudhui ni kama sahani na chakula. Sahani yaweza kutengwa na chakula pale ambapo chakula hicho kitaondolewa. Penina Muhando anasema, chakula ndio maudhui yaani umbo la ndani la kazi ya fasihi na sahani ndio fani ambayo ni umbo la nje la kazi ya fasihi. Hivyo yeye anaona kuwa fani na maudhui ni dhana mbili ambazo zinaweza kutenganishwa na bila athari yoyote.
Naye T. Sengho anasema kuwa fani na maudhui ni kama chungwa na ganda, akiwa na maana kuwa chungwa ndio maudhui na ganda ndio fani. Hapa T. Sengho anatoa msimamo kuwa fani na maudhui vinaweza kutenganishwa bila ya athari, kwani chungwa linaweza kutengwa na ganda lake.
Mtaalam mwingine anayeegemea mtazamo wa kidhanifu anasema kuwa fani na maudhui ni kama kikombe na chai. Huyu ni Mtaalam F. Nkwera ambaye anasema kuwa chai ndio maudhui na fani ndio kikombe. Hapa F. Nkwera anataadharisha kuwa chai inaweza kunywewa kwenye kikombe na kikombe kubakia kitupu, hivyo fani yaweza kutengwa na maudhui kama vile chai inavyoweza kutengwa na kikombe.
Katika mtazamo wa kiyakinifu, Senkoro anasema kuwa fani na maudhui ni sawa na sarafu. Hapa anamaanisha kuwa fani na maudhui ni dhana mbili zisizoweza kutenganishwa kama vile pande mbili za sarafu moja.
Senkoro F. E. M. K. anasisitiza kuwa fani na maudhui havitenganishiki bali hutegemeana ili kazi ya fasihi iweze kuwa bora zaidi. Kazi ya fasihi ambayo maudhui yamezidi fani huwa chapwa au fani ikizidi maudhui, kazi hiyo ya fasihi huwa chapwa, hivyo maudhui na fani ni dhana ambazo hutemeana. Fani na maudhui lazima vilingane na kushabihiana ili kazi yenyewe iweze kuwa bora na yenye mvuto zaidi.
Mtazamo mwingine unadai kuwa fani na maudhui hulinganishwa na roho na mwili ambapo haiwezi kutenganishwa na mwili kwani kwa kufanya hivyo athari itakayotokea ni kwamba mwili hautaweza kufanyakazi ipasavyo pasipo roho.
Vilevile tunaweza kufananisha fani na maudhui kama gari na injini. Hii ni dhana ambayo inajidhihirisha kuwa gari haliwezi kutenda bila injini, hivyo ni kuweza kuthibitisha kuwa fani na maudhui ni dhana mbili zisizotenganishwa kwani huleta athari zinapotenganishwa na vilevile fani na maudhui hutenda kazi pamoja.

UKUMUSHAJI


SWALI” Jadili dhana ya ukumushaji na sifa zake kwa kutumia mifano sahihi.

UKUMUSHAJI
Ni dhana ambayo hutoa maelezo zaidi au
Ya ziada kuhusu nomino, kivumishi, kitenzi, kielezi au kikundi cha maneno
KIKUMISHI
Ni neno , kirai au kishazi ambacho hutoa maelezo ya ziada kuhusu nomino, kivumishi, kitenzi, kielezi au kikundi cha maneno. Aidha, kikumushi huweza kuwa sentensi itoayo maelezo zaidi kuhusu sentensi nyingine.
Mfano.
Mtoto aliyekuja juzi ameondoka.
Katika sentensi hii kishazi tegemezi “ aliye kuja juzi” ni kikumushi ambacho kinatoa maelezo ya ziada kuhusu nomino “ mtoto:.
Mwanafunzi mrefu sana ameanguka.;
Neno “sana” ni kikumushi kinachotoa maelezo ya ziada kuhusu kivumishi “ mrefu”
Mifano zaidi
Gari lilikimbia kwa kasi sana
Maduhu anaimba vizuri mno
Ninapenda unavyosema.
Mwalimu aliye kwenda dukani jana amerudi.
Kimsing ukumushaji ni dhana pana zaidi ya uvumishi, kwani ukumushaji hutoa maelelezo zaidi kuliko uvumishaji. Pia kivumishi kipo katika kategoria ya kileksika lakini kikumushi kipo katika kategoria amilifu ya isimu miundo


MAZINGIRA YA UTOKEAJI WA UKUMUSHAJI
Ukumushaji unaweza kutokea baada ya nomino
Kwa mfano:
Kitabu kizuri kimepotea

Wanafunzi wapole wamefaulu mitihani yao vizuri

Askari katili ameuwa

Kijana mtiifu amezadiwa kitabu
Baada ya kiwakilsishi pia kikumishi kinaweza kutokea
Kwa mfano
Wale watundu wamefukuzwa shule

Yule msafi ameondoka chuoni
Kikumishi huweza kutokea baada ya kivumishi
Kwa mfano
Mwanafunzi mrefu kuliko wote ameanguka

Mwimbaji mashuhuri sana amekodiwa Uganda

Mwalimu mlevi kupindukia ameachishwa kazi.
Vivyo hivyo kikumishi huweza kutokea baada ya kielezi
Kwa mfano
Juma anaimba vizuri

Mbwa mkali amejeruhiwa sana

Ninapenda anavyocheza

Mwanariadha anakimbia kwa kasi
Ukumushaji vilevile huweza kutokea baada ya kielezi
Kwa mfano
Juma anaimba polepole mno

Mharifu amejitetea vizuri sana

Mwanafunzi amewasilisha kazi kwa ujasili mwingi
Ukumushaji pia huweza kutokea baada ya kihusishi
Kwa mfano
Janeth anakula wali kwa mkono

Juma amekaa juu ya meza

Maria analia kwa uchungu

SIFA ZA UKUMUSHAJI
Hutoa maelezo ya ziada kuhusu nomino, kivumishi, kitenzi au kikundi cha maneno
Mfano:
Mvulana mwembamba amepotea
Neno “ Mwembamaba” ni kikumushi kinachotoa maelezo ya ziada kuhusu nomino “ mvulana”
Kijana mnene sana anacheka.
Neno “sana” ni kikumushi kinachotoa maelezo ya ziada kuhusu “kivumishi” mnene
Ninapenda unavyocheza
Neno “ unavyocheza “ ni kikumishi kinachotoa malelezo ya ziada kuhusu “ kitenzi” “Ninapenda”.
Mwalimu aliyekuja jana asubuhi ameondoka.
Neno “aliyekuja jana asubuhi” ni kikumushi kinachotoa maelezo ya ziada kuhusu nomino “ mwalimu”
Mchungaji anahubiri vizuri sana
Neno “ sana” ni kikumushi kinachotoa maelezo ya ziada kuhusu kielezi “ vizuri”
Kikumushi kinaweza kuondolewa kwenye tungo bila kupoteza maana ya msingi ya tungo hiyo.
Mfano
Mtoto mzuri amerudi
mtoto amerudi
Ninapenda unavyokula
Ninapenda
kikumushi huweza kuundwa na neno moja au kikundi cha maneno.
Mfano
mtoto anacheza vizuri sana (neno moja)

Msichana aliyekaa mbele yangu ni msafi (kikundi cha maneno)

Kikumushi kipo katika kategoria amilifu ya isimu miundo ( mpangilio wa maneno katika tungo).
Mfano.
Msichana mrembo sana anacheka

Msichana mrembo anacheka
Kikumushi kinaweza kutokea mara moja au zaidi katika tungo
Mfano:
Ng’ombe aliyepotea jana asubuhi amepatikana leo asubuhi

Msichana anacheza vizuri sana na Baba analima vizuri sana.
Ukumushaji huweza kutokea kwenye kiima au kiarifu au pande zote kwa wakati mmoja
Mfano
Mvulana aliyetumwa kwenda kumletea mgonjwa dawa amerudi mapema mno.

Kijana aliyepotea jana ameonekana

Juma anatembea kwa madaha sana
Ukumushaji huweza kutokea katika sentensi changamano ambapo kishazi tegemezi huchukua nafasi ya kikumushi
Kwa mfano
Kijana aliyekuja jana ameondoka leo asubuhi

Mbuzi aliyezalia porini ameletwa nyumbani

Kitabu kilichoibiwa kimerudishwa

Nyimbo zilizoimbwa zinafurahisha
Kwa ujumla dhana ya ukumushaji na uvumishaji kwa jinsi tulivyojadili ni dhana ambazo zinafanana katika utendaji kazi wake lakini upekee wa ukumushaji ni kwamba huweza kutokea katika kikundi nomino pekee.
Hivyo basi ukumushaji ni mpana zaidi kuliko uvumishaji.



MAREJELEO
Matinde, S.R (2012) Dafina ya lugha, Isimu na Nadharia, Mwanza: Serengeti Educational Publishers (T) Ltd
Habwe, J na Karanja, P, (2004). Misingi ya sarufi ya Kiswahili; Nairobi- Kenya: phoenix publishers Ltd

Jumapili, 18 Mei 2014

MIKABALA YA TAALUMA YA SARUFI.


MIKABALA YA TAALUMA YA SARUFI.


(a) Sarufi ubongo
(b) Sarufi kama kaida za kiisimu.
(c) Sarufi kama tafiti na uchambuzi wa miundo inavyooneka kwenye lugha.

UTANGULIZI WETU UTAZINGATIA MAMBO YAFUATAYO.

· Maana ya sarufi.
· Mkabala wa kimapokeo.
· Mkabala wa kisasa.

MJADALA WETU UTAJIKITA KATIKA VIPENGELE VIFUATAVYO


Ufafanuzi wa sarufi ubongo
Ufafanuzi wa sarufi kama kaida za kiisimu
Ufafanuzi wa sarufi kama tafiti na uchambuzi wa miundo inavyooneka kwenye lugha.
Tofauti zilizopo katika mikabala hii.

Katika mjadala huu, kwanza kabisa tutaanza kwa kuangalia dhana muhimu ambazo zimejitokeza katika mada yetu, ambazo ni sarufi, mkabala wa kimapokeo pamoja na mkabala wa kisasa. Kisha tutangalia kwa kujadili kiini cha mada, ambapo tutaangalia jinsi sarufi ubongo, sarufi kama kaida za kiisimu na sarufi kama tafiti na uchambuzi wa miundo inavyooneka kwenye lugha na inaangukia katika mkabala upi na inatofautiana vipi.
Tukianza na maana ya sarufi kwa mujibu wa wataalamu mbalimbali kama vile:-
Kihore na wenzake (2005) wakimnukuu Gaynor (1968:88), wanaeleza kuwa sarufi ni sayansi ya muundo wa lugha pamoja na sheria, kanuni na matumizi yake ambayo kwa kawaida hukubalika kwa watumiaji wake.
Vile vile Mdee (1999) anafasili sarufi kama mfumo wa kanuni za lugha zinazomwezesha mzungumzaji kutunga sentensi nyingi sahihi na zenye kukubaliwa na wazawa wa lugha.
Pia Massamba na wenzake (1999:31) katika mtazamo wa pili wa kufasili dhana ya sarufi wanaeleza kuwa sarufi ni kanuni sheria au taratibu za uchambuzi zinazotawala lugha.
Hivyo basi wanasarufi hawa wanaonekana kukubaliana kwamba sarufi ni kanuni, sheria na taratibu zinazotawala lugha. Lakini kwa kiasi kikubwa tunakubaliana na fasili iliyotolewa na Mdee kutokana na kwamba ameweza kutufafanulia vizuri kanuni hizo na taratibu za lugha ndizo zinazomwezesha mzungumzaji kutunga sentensi nyingi, sahihi na zenye kukubaliwa na wazawa wa lugha.

Kwa mfano:- sentensi za kiswahili zina muundo wa
N + V + T + E
Mtoto mzuri anacheza uwanjani.
N V T E
Baada ya kuangalia dhana ya sarufi kwa mujibu wa wataalamu mbalimbali sasa tunaweza kuangalia mikabala mikuu miwili ya sarufi ambayo ni:-
i. Mkabala wa kimapokeo
ii. Mkabala wa kisasa.
Kwa kuanza na mkabala wa kimapokeo kwa mujibu Khamisi na Kiango (2002), wanaeleza kuwa hii ni sarufi ya kale, wataalamu wanaohusishwa na mkabala huu walijitokeza kuanzia karne ya 5 kabla ya kristo na katika karne ya 18 na karne ya 19 baada ya kristo, wataalamu hao ni kama vile Plato, Aristotle, Panin, Protagoras ambao walijihusisha na lugha kwa kutaka kujua asili yake ikiwa ni sehemu ya uchunguzi wa asili ya maumbo hususani walitaka kujua kama lugha ni tukio la maumbile au tukio la unasibu.
Pia Massamba na wenzake (wameshatajwa) wanaeleza kwamba sarufi mapokeo zilikuwa ni sarufi elekezi ambazo zilisisitiza kanuni na nini cha kusema na wajua lugha. Watu wasiojua kanuni za lugha wanapaswa kujifunza kutoka kwa wanaojua sarufi ya lugha. Wanaendelea kusema kuwa, wanaojua lugha hupaswa kutunga kanuni za sarufi.

Vile vile Habwe na Karanja (2004:124), wanadai kuwa mitazamo hii ya wanasarufi hawa wa kimapokeo iliathiri mbinu na njia za kuangalia lugha kwani sarufi mapokeo ilijikita katika lugha za kiulaya kama vile kiyunani na kilatini.

Sifa mbalimbali za lugha hizi ambazo ziliaminiwa kuwa bora, zilichunguza kilatini na kiyunani zilielezwa kuwa ni lugha duni na kutwezwa na kudhalilishwa
Sarufi mapokeo ilielekeza watu jinsi ya kutumia lugha, uelekezi huo hata hivyo ulijikita kwenye sheria za lugha ya kilatini kwa mfano sentensi haikupaswa kuishia na kihusishi wala kuanza na kiunganishi.
Udhaifu mkubwa wa sarufi mapokeo ni kwamba, taratibu za uchanganuzi wa lugha hazikuzingatia lugha ya kuzungumza kama ilivyo leo. Wanasarufi mapokeo walienzi na kuchunguza lugha ya maandishi. Hivyo basi ni dhahiri kwamba mkabala huu unaangukia katika mitazamo ya kifalsafa.
Hivyo basi ni wazi kuwa katika sarufi hii ya mapokeo tunakutana na mikabala miwili inayoangukia katika mkabala huu ambayo ni sarufi ubongo na sarufi kama kaida za kiisimu.
Mkabala wa pili, ni mkabala wa kisasa, unaoongozwa na wanasosiolojia ambao unahusisha sarufi mbalimbali kama vile :-

i. Sarufi msonge
ii. Sarufi miundo virai
iii. Sarufi geuza maumbo zalishi
iv. Sarufi husiano

Katika mkabala huu ndipo tunapata mkabala wa sarufi kama tafiti na uchambuzi wa miundo inavyooneka kwenye lugha.
Hivyo basi baada ya kujadili mikabala mikuu miwili ambayo ni mkabala wa kimapokeo na mkabala wa kisasa, zifuatazo ni sifa muhimu za sarufi ubongo, sarufi kama kaida za kiisimu na sarufi kama tafiti na uchambuzi wa miundo inavyooneka kwenye lugha ambazo kwazo tutaona jinsi kila moja inavyotofautiana na nyingine.
Kwa kuanza na sarufi ubongo, kwa mujibu wa Nordquist (2012), anaeleza kuwa sarufi ubongo ni sarufi endelevu ambayo inamwezesha binadamu kuzalisha lugha ambayo inaweza kueleweka kwa wengine

Pia Sharpe (2006), anaeleza kuwa sarufi hii hufananishwa na umilisi, anaendelea kueleza kuwa sarufi hii humwezesha mtu kuweza kusikia na kutambua kama sentensi hiyo ni sahihi au si sahihi.
Chomsky (1957), anaeleza kuwa kila binadamu amezaliwa na uwezo wa kuzalisha tungo mbalimbali zisizo na ukomo ambazo humpatia uwezo au uzoefu wa sarufi ya lugha. Pia anafafanua kwamba kila binadamu huzaliwa na kifaa katika ubongo wake ambacho kinamwezesha kuamili lugha ya aina yoyote, amekiita kifaa cha uamiliaji lugha (KIULU). Kwa mfano mtoto mdogo mwenye umri chini ya miaka saba anaweza kuamili lugha yoyote na mahali popote.

Mgullu (1999), anaeleza kuwa sarufi ubongo huchunguza jinsi binadamu anavyojifunza lugha kwa mfano hatua mbalimbali ambazo hupitia wakati anajifunza lugha yake ya kwanza.
Kwa hiyo tunakubaliana na fasili zote zilizotolewa na wataalamu hapo juu kutokana na kwamba sarufi ubongo, hii ni sarufi ambayo inachunguza jinsi binadamu anavyoweza kuamili lugha na kujifunza lugha pia kuweza kuzalisha sentensi mbalimbali ambazo anaweza kuzitumia katika mawasiliano.
Vile vile wataalamu wa mkabala huu hueleza kuwa upo uhusiano mkubwa kati ya akili, kufikiri na lugha bila shaka uhusiano huu ni ule wa taathira ya lugha yaani dhana inayoeleza kuwa kwa kawaida kila lugha huathiri watumiaji wake kwa kiasi kikubwa.
Vile vile wataalamu wa mkabala huu wanaeleza jinsi watu wanavyojifunza lugha ya pili au lugha ya tatu.
Kwa kifupi mkabala huu hujihusisha na mambo kadha kama vile:-
(i) Kumwezesha binadamu kuweza kuzalisha au kutunga sentensi mbalimbali.
(ii) Sarufi ubongo huusika na uamiliaji wa lugha na ujifunzaji wa lugha.
(iii) Sarufi hii huwakilisha maarifa ya mzungumzaji wa lugha (umilisi alionao mzungumzaji).
Mkabala mwingine wa sarufi ambao unaangukia katika mkabala wa sarufi mapokeo ni sarufi kama kaida za kiisimu.
Kwa mujibu wa Encyclopedia (1970), wanaeleza kuwa sarufi kaida ni mpangilio unaoonyesha au kueleza kanuni za kisarufi katika lugha ambazo hushughulika na kanuni za uundaji wa maneno, maumbo ya maneno, miundo ya maneno, miundo ya sentensi, vile vile inahusisha taarifa maalumu kuhusu fonetiki na fonolojia (taaluma inayohusika na utamkaji sahihi unaokubalika)
Pia kwa mujibu wa Babylon Dictionary (1997), wanaeleza kuwa sarufi kaida ni mfumo wa kisarufi ambao unafafanua kipi sahihi na kipi si sahihi katika lugha, pindi mzungumzaji anapozungumza, amezungumza sahihi au si sahihi.
Kwa hiyo tunaweza kueleza kuwa sarufi kaida hujishughulisha sana na:-
i. Kuelekeza namna ya matumizi sahihi ya lugha.
ii. Wataalamu wa lugha ndio wanaounda kanuni na miongozo ya lugha ambayo inatakiwa kufuatwa na wale wasiojua lugha.
Kwa mfano:- kanuni mojawapo ya miundo ya sentensi za Kiswahili huwa na muundo wa kiima na kiarifu.
Vile vile sentensi nyingi za Kiswahili huwa na muundo wa kirai nomino na kirai kitenzi.
Hivyo basi katika mkabala huu wa sarufi watu wasiojua lugha wanapaswa kufuata kanuni na taratibu zilizoundwa na wanaojua lugha kwa mfano wanasarufi.
Pia mkabala mwingine wa sarufi ambao unaangukia katika mkabala wa kisasa ni sarufi kama utafiti na uchambuzi wa miundo inayoonekana katika lugha.
Kwa mujibu wa Besha (2007), anaeleza kuwa huu ni mkabala unaohusika hasa na uchambuzi wa muundo wa lugha, sauti za lugha, muundo wa sentensi na hata maana za tungo za lugha.
Pia mgullu (1999), anaeleza kuwa lengo la mkabala huu ni kufafanua vipengele vyote vya lugha fulani kama vilivyo hivi sasa au vilivyokuwa wakati fulani.
Hivyo basi Besha na Mgullu wanakubaliana kuwa huu ni mkabala unaofafanua namna au jinsi watu wanavyozungumza lugha na sio kuwaelekeza waizungumze vipi lugha yao.
Hivyo basi kwa ujumla mkabala huu unajihusisha na mamba yafuatayo:-
i. Hautilii mkazo mabadiliko yaliyotokea katika lugha hata kama mabasiliko hayo yapo.
ii. Mkabala huu hauamuru watu waseme vipi na vipi wasiseme.
Kutokana na sifa mbalimbali zilizojitokeza katika mikabala hii, tumeweza kubaini tofauti zilizopo baina ya mikabala hii mitatu ambazo ni kama zifuatazo:-
Sarufi ubongo, sarufi kama kaida za kiisimu zinajitokeza katika mkabala wa kimapokeo wakati sarufi kama tafiti na uchambuzi wa miundo inavyooneka kwenye lugha inajitokeza katika mkabala wa kisasa.
Vilevile sarufi ubongo humwezesha binadamu kuweza kuzalisha miundo mbalimbali ya tungo wakati sarufi kama kaida za kiisimu haijihusishi kabisa na masuala ya ubongo bali yenyewe hujihusisha na mazoea ya kawaida ya watumiaji wa lugha ambapo kunakuwa na makosa ambayo huwafanya wataalamu kuunda kanuni za lugha ambazo zinatakiwa kufuatwa na wasiojua lugha hii inatofautiana na sarufi kama tafiti na uchambuzi wa miundo inavyoonekana kwenye lugha kwa kuwa haihusiani na masuala ya ubongo wala kaida, bali yenyewe hujihusisha na utafiti na ufafanuzi wa miundo ya lugha kama inavyotumika na wazungumzaji wa lugha na haiwaelekezi jinsi ya kuzungumza.
Kwa kuhitimisha tunaweza kusema kwamba pamoja na tofauti hizo zilizojitokeza katika mikabala hiyo mitatu, mikabala hii inaonekana kufanana kwani yote inajihusisha na lugha ya binadamu, pia mikabala hii imechangia kwa kiasi kikubwa katika maendeleo ya taaluma ya isimu na ndio imekuwa darajia kwa wataalamu mbalimbali katika kufanya tafiti zao kwa mfano baada ya kushindwa kwa sarufi ubongo na sarufi kama kaida za kiisimu ndipo kukazaliwa kwa sarufi kama tafiti na uchambuzi wa miundo inavyooneka kwenye lugha.

MAREJELEO
Babylon Dictionary. (1997). Translation and Information Platform. Babylon Ltd.
Besha, R.M. (2007). Utangulizi wa lugha na Isimu. Macmillan Aidan Ltd. Dar es Salaam.
Chomsky, N. (1957). Syntactic Structures. Mouton The Hague.
Khamis, A.M na John G.K (2002). Uchanganuzi wa sarufi ya Kiswahili. TUKI. Dar es salaam.
Habwe, J na Peter K (2007). Msingi ya sarufi ya Kiswahili.Phoenix Publishers. Nairobi.
Kihore, Y.M na wenzake. (2008). Sarufi Maumbo ya Kiswahili Sanifu (SAMAKISA):Sekondari na Vyuo. TUKI. Dar es Salaam.

Massamba, D.P.B. na wenzake. (2009). Sarufi Miundo ya Kiswahili Sanifu (SAMIKISA): Sekondari na Vyuo. TUKI.

SENTENSI ZA KISWAHILI.


Sentensi za Kiswahili


Sentensi ni kundi la neno moja au maneno zaidi yenye kiima na kiarifa na inayofuata kanuni za sarufi.


Angalia:


Muundo wa Sentensi => Kikundi Nomino(KN)/Kiima, Kikundi Tenzi(KT)/Kiarifa, Shamirisho na Chagizo


Virai na Vishazi


Uchanganuzi wa Sentensi Sahili



Aina za Sentensi


1. Sentensi Sahili



Hizi ni sentensi zenye kishazi kimoja na huwakilisha wazo moja tu.


Sentensi sahili kutokana na kikundi tenzi pekee:


Ninasoma => KT(T)


Hajakuandikia barua => KT(T + N)


Tulimwona nyoka mkubwa = >KT(T + N + V)


Alikimbia haraka sana => KT(T + E + E)


Kikundi Nomino + Kikundi Tenzi


Sakina anaimba. => KN(N) + KT(T)


Latifa na Kanita wamejipamba vizuri. => KN(N + U + N) + KT(T + E)


Jua kali liliwaka mchana kutwa. => KN(N + V) + KT(T + E + E)


Runinga ya Bwana Kazito imeharibika tena. => KN (N + V + N + N) + KT (T + E)



2. Sentensi Ambatano.


          Sentensi ambatano ni sentensi zenye zaidi ya kishazi huru kimoja na huwakilisha mawazo mawili au zaidi. Aghalabu sentensi hizi hutumia viunganishi(U) au alama za uakifishaji kama vile kituo(,) na nukta-nusu (;) ili kubainisha wazo moja toka nyingine.


Kuunganisha Sentensi Mbili:


Chesi alisoma kwa bidii. Chesi alianguka mtihani.


=>Ingawa alisoma kwa bidii, Chesi alianguka mtihani.


Dadangu amerudi nyumbani. Dadangu amelala.


=>Dadangu amefika nyumbani na kulala.


Mifano mingine:


Tulifika, tukaona, tukapiga na tukatawala.


Leo inaonekana Karimi amejipamba akapambika.


Angalia: Uchanganuzi wa Sentensi Ambatano


3. Sentensi Changamano.


Hizi ni sentensi zinazoundwa kwa kuunganisha kishazi huru pamoja na kishazi tegemezi au sentensi mbili kwa kutumia o-rejeshi ili kuleta zaidi ya wazo moja.


Kuunganisha Sentensi:


Juma amenilitelea kitabu. Nilikuwa nimetafuta kitabu hicho kwa muda mrefu.


=> Juma ameniletea kitabu ambacho nilikuwa nimekitafuta kwa muda mrefu.


Yeye ni mwizi. Alipigwa jana jioni.


=> Yeye ndiye mwizi aliyepigwa jana jioni.


Mifano Zaidi:


Nimemuona yule ninayemtafuta na neema zake.


Ndoto zinazotisha ni za kishetani.


Angalia: Uchanganuzi wa Sentensi Changamano


Tanbihi: Ili kutofautisha sentensi ambatano na changamano kwa urahisi, sentensi changamano hutumia o-rejeshi (k.m ambacho, ambaye, niliye- , nililo- n.k)

MOFOLOJIA YA KISWAHILI.



Mofolojia ya Kiswahili


Mofolojia ya kiswahili


· Malengo ya somo hili • Kueleza na kufafanua maana ya mofolojia • Kutambua na kufafanua zaidi mofolojia na vipashio vyake.


· Kunihusu mimi • STEPHEN MANYAMA CHARLES • MWANAFUNZI WA CHUO KIKUU CHA ARUSHA,NI MWALIMU-MWANAFUNZI WA SOMO LA KISWAHILI KWA VYUO NA SEKONDARI,Karibuni kwa Mchango na Mawazo na hata kwa kujifunza pia.

· Utangulizi • Maana ya mofolojia


· Maana ya mofolojia • Mofolojia ni tafsiri ya neon la kiingereza “Morphology”. Neno hili nalo linatokana na neon la kiyunani “Morphe” lenye maana ya muundo au umbo ( Aurbach et al 1971; 106). • Mofolojia ni neno linalotumiwa kumaanisha utanzu wa isimu unaoshughulikia muundo wa maneno ( Habwe na Karanja 2004).


· Maana.......... • Hartman (1972). Mofolojia ni tawi la sarufi ambalo hushughulika na uchunguzi na uchambuzi wa maumbo, fani na aina za maneno yalivyo sasa pamoja na historia zake


· Maana......... • Kwa ujumla mofolojia ni taaluma inayoshughulikia lugha pamoja na mpangilio wake katika uundaji wa maneno. Vipashio hivyo vya lugha huitwa mofimu


· Uhusiano uliopo kati ya mofolojia na matawi mengine ya sarufi • Mofolojia na fonolojia • Kuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya mofolojia na fonolojia:i. Vipashio vya kifonolojia ndivyo hutumika katika kuunda vipashio vya kimofolojia mfano


· Mofolojia na fonolojia • Vipashio vya mofolojia ni fonimu, mfuatano wa fonimu ndio huuna vipashio vya kimofolojia ambavyo ni mofimu Mfano • Fonimu: i, p, t, a, huunda • mofimu: Pit-a • Hivyo basi neno pita limeundwa na mofimu mbili na fonimu nne


· Mofolojia na fonolojia ii) Uhusiano mwingine kati ya fonolojia na mofolojia ni kwamba, kanuni za kifonolojia hutumika kueleza maumbo ya kimofolojia ambayo yanaathiriana. Mfano Katika neno mu-ana mwu-alimu


· Mofolojia na fonolojia • Kipashio [mu] katika mifano hapo juu kinajitokeza kama [mw-] inapofuatwa na irabu ambayo. Mu mw-/-I


· Neno hutumika kuundia sentensiØMofolojia na sintaksia i. Vipashio vya msingi vya kimofolojia ndivyo hutumika katika kuundia daraja hili la sintaksia.·


Mwisho kwa asante usomaji Mawasiliano: charlesmanyama@rocketmail.com,0768326604 ©2014

· Maswali na majibu • Kwa maswali au mchango wowote kuhusuiana na kiswahili nifuate kwenye email yangu ya charlesmanyama@rocketmail.com