Subcribe to our RSS feeds Join Us on Facebook Follow us on Twitter Add to Circles

Jumanne, 4 Novemba 2014

UAMILIAJI LUGHA

UAMILIAJI LUGHA SARUFI MAJUMUI NA UAMILIAJI LUGHA YA PILI.
 Makala haya yataangalia maana ya sarufi majumui, masuala ya msingi yanayohusu maarifa ya lugha, sifa za sarufi majumui, sarufi majumui na uamiliaji lugha ya pili na mwisho tathmini. Kwa mujibu wa Chomsky (1976:29) kama alivyonukuliwa na Ellis (1996:430) sarufi majumui ni mfumo wa kanuni na sheria ambazo ni msingi wa lugha za binadamu (tafsiri yangu). Muasisi wa nadharia hii ni Noam Chomsky. Msingi wa nadharia hii ni kwamba binadamu anapozaliwa anakuwa na maarifa asilia ambayo humsaidia katika ujifunzaji lugha; mambo ya ndani na nje ambao husaidia katika uamiliaji wa lugha. Maarifa haya hupatikana pale tu binadamu anapozaliwa kwani huwa na kifaa cha uamiliaji lugha ambacho kinakuwa na kanuni majumui na kanuni badilifu ambazo hukutana na tajiriba (uwezo wa jamii katika lugha) na kusababisha uamiliajli lugha kutokea. Waamiliaji wa lugha ya kwanza huwa na maarifa asilia ambayo huwawezesha kuiamili lugha yao kwa kutumia maarifa hayo. Hivyo maarifa hayo yanaamshwa na tajiriba ambayo mjifunzaji anaikuta katika jamii iliyomzunguka na hatimaye kukutana na maarifa asilia katika kifaa cha uamiliaji lugha hatimaye kuzalisha sarufi mahsusi ya lugha husika. Waamiliaji wa lugha ya pili wanakuwa na lugha ya kwanza ambapo sifa za sarufi majumui bado humwezesha kuamili lugha ya pili, kwani kanuni badilifu na kanuni majumui zilizojengwa kwa misingi ya lugha ya kwanza hutumika katika kuamilia lugha ya pili. Hivyo kwa mujibu wa nadharia ya sarufi majumui inamsaidia mjifunzaji katika kuamili lugha ya pili. Wataalam mbalimbali wameweza kujadili juu ya uwezo wa sarufi majumui wa kuwa kifaa weazeshi cha kujifunza lugha ya pili, kuna wataalam wanaokubali na wanaokataa mchango huo. Kama Flyn (1984-1987) anavyoelezea kama alivyonukuliwa na Ellis (1996:453) kifaa cha uamiliaji lugha ya kwanza kitahusika na mchakato  wa ujifunzaji lugha ya pili. Akaendelea kusema kanuni badilifu za lugha ya kwanza na lugha ya pili zikiwa sawa ujifunzaji utakuwa rahisi kwa sababu mjifunzaji wa lugha ya pili ana uwezo wa kuhusisha miundo wakati kanuni hizo zikitofautiana kati ya lugha ya kwanza na lugha ya pili ni vigumu kujifunza. Flyin yeye anaunga mkono juu ya sarufi majumui kuwa kifaa wezeshi katika ujifunzaji wa lugha ya pili. Kwani anaamini bado maarifa ambayo mjifunzaji wa lugha ya kwanza anayoyatumia katika ujifunzaji wa lugha hiyo, ndiyo yale yale anayoyatumia mjifunzaji wa lugha ya pili. Hata hivyo Clahsen na Muysken (1986-1991) kama walivyonukuliwa na Ellis (1996:454) wanasema uamiliaji wa lugha ya pili ni tofauti na uamiliaji lugha ya kwanza muamiliaji lugha ya kwanza huwa na kifaa wezeshi cha uamiliaji lugha wakati wa lugha ya pili hutumia mbinu za lugha ya kwanza katika kujifunza lugha ya pili wanaendelea kusema muamiliaji lugha ya pili huhitaji nadharia ya isimu wakati wajifunzaji lugha ya pili huhitaji naharia tambuzi. Hata hivyo sarufi majumui imeangaliwa katika mitazamo tofautitofauti, hivyo kuonesha ubora lakini pia mapungufu yake katika ufundishaji wa lugha: Kwa kuwa na sarufi majumui tunaona kuwa sifa za lugha huingiliana, hivyo mwingiliano wa lugha ya kwanza na ya pili unaweza kumwezesha muamiliaji lugha ya pili pale miundo ya lugha ya kwanza na lugha ya pili itafanana na hata ikitofautiana mjifunzaji anakuwa na uwezo wa kujiundia miundo yake itakayomsaidia katika ujifunzaji wake kwa kutumia sifa majumui za lugha. Flynn (1984;1987) kama alivyonukuliwa na Ellis(1996;453) anaeleza kuwa “kifaa cha uamiliaji lugha ya kwanza kinaweza kutumika katika uamiliaji wa lugha ya pili. Kama kanuni badilifu za lugha ya kwanza na ya pili zinauhusiano hurahisisha ujifunzaji”. Hivyo yeye anakubali kabisa kuwa sarufi majumui ni kifaa wezeshi katika ujifunzaji wa lugha ya pili, anaamini sifa za mjifunzaji wa lugha ya kwanza ndizo ambazo anakuwa nazo mjifunzaji wa lugha ya pili. Aidha Ellis (1994:461) anaeleza ubora wa sarufi majumui kuwa imetoa msingi wa uibukaji wa nadharia zingine za ujifunzaji lugha baada ya kuegemea kwenye maarifa asilia anayozaliwa nayo binadamu. Pia imeweza kueleza sifa majumui za lugha mbalimbali za ulimwengu kwa ufupi, hivyo kusababisha sifa za lugha kueleweka kwa urahisi kwa wajifunzaji wa lugha ya pili. Kwa mujibu wa Ellis (1994:458) udhaifu huu unajidhihirisha katika maeneo kadhaa, kiini cha sarufi majumui yenyewe, pia mbinu zilizotumika kukusanyia data. Hivyo inaonekana kuwa kuna tatizo katika mbinu za ufundishaji na namna ya ufundishaji wa lugha ya pili. Nadharia ya sarufi majumui haikuonyesha namna gani mjifunzaji anapata ujuzi wa kutumia maarifa asilia aliyozaliwa nayo lakini pia mbinu iliyotumia katika ukusanyaji wa data ni ile mbinu ya kukusanya data isiyo ya vipindi maalum. Hivyo kupelekea data zake kutoweza aminika. Vilevile clahsen na Muysken (1986), Meisel(1991) kama walivyonukuliwa na Ellis (1996;454) muamiliaji wa lugha ya pili atakuwa tofauti na muamiliaji wa lugha ya kwanza kwa sababu kifaa cha uamiliji lugha kipo tu kwa mtu anayejifunza lugha ya kwanza na yule anayejifunza lugha ya pili huweza kusaidiwa na maarifa/mbinu mbalimbali ya ufundishaji na mazingira. Hivyo hawa wanaona kuwa safuri majumui si kifaa wezeshi katika ujifunzaji wa lugha ya pili. Kuibuka kwa nadharia zingine kunaonesha udhaifu wa nadharia ya sarufi majumui, mfano Fabisz, N.[1] Anaelezea nadharia ya uzawa iliyoasisiwa na Andersen ambayo inasisitiza juu ya urithishaji wa lugha, pia nadharia ya utamadunishi iliyoasisiwa na John Schumann (1978)inayosisitiza jinsi utamaduni wa jamii ulivyo na mchango mkubwa katika ujifunzaji lugha kwani lugha huendana na utamaduni mfano ni vigumu kujifunza lugha ya kiingereza kwa mswahili kwasababu tunatofautiana katika utamaduni hata kama utajua kiingereza hautafanana na mwingereza mzawa kwa kuwa yeye atatumia miundo ya lugha hiyo akihusisha na utamaduni wake. Hivyo katika kujifunza lugha sarufi majumui sio kifaa wezeshi pekee cha uamiliaji lugha pekee ambacho hutumika bali kuna vitu kama mazingira, motisha na urudiaji wa mara kwa mara humpelekea muamiliaji lugha ya pili kujifunza lugha ingawa kuna utofauti wa uamiliaji kuna wengine huchukua muda mrefu na wengine muda mfupi, si lazima waamiliaji wa lugha ya pili wawe na sarufi majumui inayofanana, hivyo tofauti zao wakati mwingine haziepukiki. Kama ubora na udhaifu wa sarufi majumui unavyojidhihirisha, hii inaonesha kuwa sarufi majumui peke yake haitoshi kumfanya mjifunzaji wa lugha aweze kuamili lugha ya pili vizuri, hivyo walimu wanashauriwa kutumia nadharia changamani katika ufundishaji wao wa lugha ya pili ili kumwezesha mjifunzaji wa lugha ya pili kuamili lugha hiyo vizuri. Kimsingi sarufi majumui inajidhihirisha kuwa ni kifaa wezeshi katika ujifunzaji wa lugha ya pili licha ya kuwa na udhaifu wake, haipelekei kuiondoa katika hali ya uwezeshi katika ujifunzaji wa lugha ya pili, kwani sifa majumui zinazopatikana katika lugha mbali kwa kiasi kikubwa zinawasaidia wajifunzaji kujifunza lugha ya pili, mfano wajifunzaji wanapogundua miundo ya lugha na uundaji wa misamiati unaolingana itawawia rahisi katika ujifunzaji wao. Lakini hata ikitofautiana sarufi majumui imefafanua namna ambavyo mjifunzaji huyu ataweza kujiundia sarufi yake ambayo itakuwa imejengeka kwa misingi ya lugha ya kwanza. Kuna umuhimu wa kuwa na mazingira bora ya ujifunzaji ambapo mawasiliano yanapewa msisitizo mkubwa katika nadharia mbalimbali, hivyo walimu hawana budi kujenga mazingira hayo kwa wanafunzi wao ili waweze kujifunza lugha ya pili kwa usahihi. Ikiwa ni pamoja na kubadilisha mazingira ya darasa kuwa mazingira rafiki kwa mwanafunzi ambapo mawasiliano ndiyo kiini cha ujifunzaji. Nadharia ya sarufi majumui imeonekana ina mchango mkubwa katika tendo la ujifunzaji, lakini haitoshi kusema ndiyo nadharia pekee ambayo inapaswa kutumiwa na walimu katika ufundishaji wao kwani pia imeonekana kuwa na udhaifu, hivyo nadharia zingine kama za utamadunishi, uzawa na urithishaji ni muhimu kuzipa umuhimu pia ili tendo zima la kujifunza liweze fanyika, lakini pia cha msingi ni kujua wajifunzaji hawawezi kuwa na uwelewa wa aina moja hata kama haya yote yatatimia, hivyo kinachoangaliwa ni kufikia ile hali ya kawaida katika matumizi ya lugha, ambapo kila mjifunzaji anatarajiwa afikie.

MAREJEO
Ellis, R. (1994), Second Language Acquisition, USA: Oxford University Press Fabisz, N. ANALYSIS OF KRASHEN’S THEORY OF SECOND LANGUAGEACQUISITION,http://webspace.webring.com/people/ap/panandrew/sla.html,

ISTILAHI

 Externa approach  - mkabala wa nje
Intuition              - ujuzi
 Internar approach  - mkabala wa ndani
Parameter             - kanuni badilifu
Principles             - kanuni majumui
 Prompted              - Papo hapo

Universal grammar - sarufi majumui 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni